Takribani bunduki 90 ambazo zilikuwa zikimiliwa na watu kinyume cha sheria zimesalimishwa kwa maafisa wa polisi katika kaunti ya Tana River.
hatua hiyo imetokana na oparesheni ya kiusalama iliyofanywa na maafisa wa polisi ambayo inaendelezwa hadi sasa katika maeneo ya Tana Kaskazini na Bangale kutokana na vita vya kikabila ambavyo vimekuwa vikishuhudiwa katika maeneo hayo.
Vita vya kikabila katika eneo la Bangale kaunti ya Tana River, mara nyingi hutokea kati ya jamii za wafugaji kama vile jamii za Wardey, Degodia na Orma huku serikali kupitia idara ya usalama ikiingilia kati ili kuhakikisha jamii hizo zinaishi kwa amani.
Mizozo hii huibuka hasa kutokana na ushindani wa kupata malisho na maji kwa ajili ya mifugo wao, mizozo ya ardhi, na uchochezi wa kisiasa kuelekea chaguzi.
Serikali imezitaka jamii hizo kuzidi kuwasilisha silaha zote kwa maafisa wa polisi, ili kuzuia vita vya kila mara sawa na kuchangia amani na umoja katika jamii hizo.
Kwa muda mrefu kaunti ya Tana River imekuwa ikishuhudia vita vya kikabila kila mara kwa mara kutokana na umiliki haramu wa silaha hali ambayo imechangia usalama wa kaunti hiyo kuwa duni.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
