Gavana wa kaunti ya Bungoma Kenneth Lusaka, amefutilia mbali baraza lake la mawaziri akilenga kulifanyia mabadiliko ili kuimarisha utendakazi wa serikali ya kaunti hiyo.
Katika taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya bahari na kutiwa saini na Gavana huyo, imebaini kwamba Katibu wa kaunti pamoja na Mwanasheria mkuu wa kaunti pia wamesimamishwa kazi, hatua hii ikitekelezwa miezi michache tu kabla ya uchaguzi mkuu ujao mwaka wa 2027.
Katika taarifa hiyo iliyotolewa na serikali ya kaunti hiyo, Gavana Lusaka alieleza kwamba hatua hiyo imetokana na utendakazi duni wa viongozi hao pamoja na kutofikia malengo ya wananchi kwa kuambatana na ajenda za Gavana huyo.
Gavana Lusaka alisema kwa kuzingatia kipengele cha 40 ibara ya kwanza sehemu ya {a}, ambayo inampa mamlaka ya kuwasimamisha kazi maafisa wakuu wa kaunti pamoja na kulivunja baraza la mawaziri, Gavana Lusaka alichukua hatua hiyo ili kuimarisha utendakazi wa kaunti.

Taarifa ya kusimamishwa kazi kwa baraza la mawaziri iliyotolewa na Gavana wa Bungoma Kenneth Lusaka
Taarifa hiyo pia ilifafanua kwamba ilichukuliwa kwa nia njema na kwa maslahi mapana ya umma, ikiongeza kwamba inalenga kuwezesha utendaji bora ndani ya utawala wa kaunti pamoja na kulinda uadilifu wa taasisi za umma.
“Nataka kuwahakikisha wakaazi wa kaunti ya Bungoma kwamba mabadiliko hayo makubwa hayataathiri huduma za kaunti kwani ni hatua moja wapo ya kuboresha utendakazi wa kaunti hiyo”, alisema Gavana.
Aidha alieleza kwamba mawasiliano zaidi kuhusu mipango ya muda na uteuzi mpya yatatolewa baadaye, kwa mujibu wa taratibu za kisheria.
Hata hivyo tetesi kutoka kwa wandani wa kisiasa, walisema kwamba hatua hiyo imechochewa kisiasa ili kuzuia mchakato uliyokuwa umepangwa wa kuwasilisha hoja bungeni ya kuwabandua uongozi baadhi ya mawaziri wa serikali ya kaunti hiyo kutokana na utendakazi duni na ufisadi.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
