Mzozo kuhusu mradi wa unyunyizaji maji wa Bura waanza upya

Mzozo kuhusu mradi wa unyunyizaji maji wa Bura waanza upya

Mradi wa unyunyizaji maji wa Bura katika kaunti ya Tanariver umeanza kushuhudia mvutano kuhusu umiliki wa ardhi.

Hii ni baada ya wakaazi wa eneo hilo kuitaka Mamlaka ya unyunyizaji maji NIA kutatua kwanza umiliki wa ardhi ya mradi huo sawa na kuweka wazi ekari za ardhi inazotumiwa kwa uendelezaji wa mradi huo wa unyunyizaji maji mashamba.

Wakaazi hao wanasema tangu mradi huo uanzishwe kumekuwa na mvutano kati ya wenyeji na mamlaka ya NIA kwani hata mipaka ya kuonyesha ardhi zinazotumika na Mamlaka hiyo imekosa kufichuliwa.

Wakaazi hao wamelalamikia kuwepo kwa njama ya kunyakuliwa kwa ardhi zao kwani serikali kuu kupitia Tume ya kitaifa ya ardhi imekosa kutoa hati miliki za ardhi kwa wakaazi wengi wa eneo hilo, hali ambayo wakihofikia kunyakuliwa kwa ardhi zao.

Wakizungumza katika kikao cha umma, wakaazi hao wamesema japo hawapingi uekezaji wa miradi ya umma ambayo itawasaidia pakubwa kujiendeleza kimaendeleo itakuwa bora zaidi iwapo mpango huo mwafaka utawekwa wazi kwa wananchi kwani ardhi inayotumika kwa mradi huo sio ya Mamlaka ya NIA.

Akizungumzia utata huo, mbunge wa Bura Yakub Adow, amelalamikia kutohusishwa na Mamlaka hiyo kuhusu ekari za ardhi ambazo zitatumika na Mamlaka hiyo, akisema kuna njama ya wananchi kunyanyaswa ardhi yao.

“Ukiangalia kwenye ramana ya ardhi utabaini kwamba ardhi hiyo ni zaidi ya ekari 170, lakini tukiwauliza mipaka ya ardhi hiii hawasema na hapo ndio inaleta shika kwa sababu wananchi wajua hii ardhi ni yao na NIA pia inatuambia kama ardhi pia ni yao, iko hadhibiti nyingi hatuelewi”, alisema Adow.

Taarifa ya Mwahoka Mtsumi